Hausigelo aliyewahi kuwaliza vijana wawili kwa mpigo na kuacha somo la kuchukua hatua

16:03:00 Unknown 0 Comments

Mara yangu kukutana na binti huyu ilikuwa ni jioni moja nikiwa nimetoka zangu kazini na nimeamua kufanya matembezi ya jioni kupitia mtaa wa pili nikijaribu kuona mambo yakoje huku nikipumzisha ubongo wangu baada ya kutumika siku nzima.

Nyumba ya tatu kutoka nyumbani kwani nikakutana na binti mmoja ambaye hakika hakunipa sana wazo la kumwangalia kwani niliona atakuwa ni msichana wa kazi ambaye baada ya majukumu yake ameamua apumzike pale kuushangaa mji wetu.

Nilimaliza matembezi yangu yaliyochukua zaidi ya saa na wakati narudi binti yule alikuwa pale pamoja na kuwa giza lilianza nikamsalimia na kuendelea na safari yangu lakini wakati huu nilimtupia jicho zaidi na kugundua kama kuna kitu kilikuwa kikimsumbua.

Sikufanya jambo lolote lakini nikaendelea na safari yangu. Siku ya pili yake muda ule ule nikapita pale lakini siku hii yule binti alionekana ni mnyonge zaidi ya jana yake na hakuwa na mtu anaongea nae, Hapa nikaanza kuhisi labda ana tatizo nikamsalimia na kuendelea na matembezi yangu.

Nilirudi nakumkuta pale pale uso wake ukiwa waonyesha kama katoka kulia baada ya mawazo makali sana niakenda nyumbani.

Nikaamua kufanya utafiti juu ya yule binti kwa siku kadhaa kwani kila nikipita alikuwa pale hata kama nisingepita kwa siku kadhaa ila siku nikipitia namwona pale.

Baada ya utafiti nikagundua anakaa mtaa wa pili kutoka pale alipokua akikaa siku zote, siku moja jioni nikapita pale nikiwa mkononi nakula pop corn na kumkaribisha alionyesha kuogopa ila akachukua na nikamuuliza jina lake na baada ya kuniambia anaitwa Miriam, nikaondoka zangu baada ya kumtania na kumwacha na tabasamu.

Nikawa natengeneza ukaribu naye kila nikipitia namwachia zawadi na kuondoka mpaka aliponizoea. Kuna siku nikaambatana na dada yangu baada ya kumsimulia kisa kizima mpaka kwa yule binti na kumkuta yupo pale pale maeneo aliyokuwa akikaa kila siku.

Tukaomba tutembee naye mpaka tukafika kwenye hoteli moja nyumba ya nane kutoka kwetu na kukaa pale. Dada alitumia zaidi ya saa akilia bila  ya kusema neno na hata juice aliyoagiziwa hakuweza kuweka hata fundo moja mdomoni na baada ya kilio aliomba arudi nyumbani kwani muda ulikuwa umefika wa kurudi nyumbani.

Tukamsindikiza na huku tukiumia kwa juhudi za kujua linalomsibu kugonga mwamba. Hatukufa moyo kwani tuliuzidisha urafiki wetu na binti yule kwa siri mpaka siku tulipofanikiwa kumweka kati na kaanza kutusimulia kisa chake.

Binti huyu alikuwa akikaa kijijini na familia yake kabla ya kifo cha baba na mama ambao walipata ajali ya basi wakiwa wanatoka mjini ambako mama alikuwa karuhusiwa kutoka hospitali baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Baada ya kifo hicho akachukuliwa na mjomba wake ambaye yeye alimleta mjini kwa ahadi za kuwa atamsomesha shule na kuchukua mzigo wa kumlea mpaka atakapohitimu mafunzo yake.

Mambo yakabadilika ambapo mjomba akaanza kumlazimisha kufanya naye ngono na mbaya zaidi kinyume na maumbile na akaivumilia ile hali kwa miezi kadhaa huku akijaribu kufanya majaribio ya kutoroka bila kufanikiwa kwani mara kwa mara baada ya majaribio hayo kushindikana alishikwa na kupigwa kipigo cha mbwa mwizi.

Akawa hana jinsi zaidi ya kuendelea kukaa pale kwani hakuwa anaruhusiwa kuwa na uhusianao na mtu yoyote hata majirani na kama ingetokea mtu akamuulizia basi ikawa balaa.Hivyo muda wa jioni ndio alipata nafasi ya kutoka na kukaa pale nje.

Lakini tukiwa tunaendelea kuongea nilihisi kitu na kumwita dada niongee nae nje, nikamwambia kila mtoto alipojaribu kukaa nilihisi kama hayuko huru kuna maumivu fulani kutokana na alivyokuwa akijilazimisha kukaa.

Dada alimchukua na kwenda kumwangalia, amini usiamini binti yule alikuwa ameharibika sehemu zake za haja kubwa na kama haitoshi kamwe usingeweza kuhimili kwa dakika hali ile jinsi dada alivyonihadithia.Pamoja na hivyo inasemekana kuwa alishashika mimba zaidi ya mara mbili na mjomba alimleta mtu na kumtoa pale nyumbani.

Siku ya pili yake kwa siri tukamchukua na kumpeleka hospitali na mara baada ya kupatiwa matibabu na kushirikisha vyombo vya dola na baadhi ya mashirika yanayotetea haki za watoto,  kufanikiwa kumshika mjomba na kumfungulia mashtaka.

Naandika haya leo kwa kuwa ni miaka 20 sasa tangu tukio hilo na binti kafanikiwa kusoma chini ya uangalizi wangu na sasa ni mfanyakazi wa shirika moja linalotetea haki za watoto hapa nchini na maisha yake ni ya furaha nami nikijivunia kuwa baba mlezi niliyechukua hatua ya kumsaidia.

Najiuliza ingekuwaje kama nisingegutushwa na ile hali na kuamua kumsaidia??

Je ni wangapi kati yetu ambao tunaweza kuhisi matatizo ya wenzetu na kuamua kuwa chachu ya kuwafanyia mabadiliko ya hali zao hata kama itagharimu au kutogharimu?

Mabadiliko uyatakayo huanza na wewe, chukua hatua sana okoa wenzako.

You Might Also Like

0 comments: