Baada ya kila dhoruba kali nuru huonekana

09:41:00 Unknown 0 Comments

Nilikulia katika kijiji kimoja kusini mwa Tanzania na mama yangu yeye alikuwa mwalimu wa chekechea wa kujitolea katika shule hiyo ya watoto wadogo pale kijijini.
Mtu niliyeambiwa kuwa ni baba yangu alikuwa ni mlevi wa kupindukia pale kijijini na fundi selemara aliyemiliki sehemu ndogo ya kufanyia kazi kama ofisi yake ya kujipatia kipato ambacho alikitumia kwa kununulia pombe na kubaki katika maisha duni sana.
Baba huyu alikuwa mkali akimpiga mama na mimi kila siku na sitaki kukumbuka jinsi kila siku mama alivyonikumbatia na tukasaidiana kulia tukimwomba Mungu ambadilishe baba huyu ambaye pia alikuwa na wake wengine wawili na kunifanya kutambua kuwa mama yangu alikuwa ni mke wa nje wa baba.
Nililia na kumwomba Mungu ayabadilishe maisha yetu kila siku na nilifurahi sana kila siku jumapili nilipomwona mama akiimba kwa furaha katika kwanya pale kanisani na kunifanya kufurahi kila ifikapo jumapili ambapo ndio nilimshuhudia mama yangu akiwa na furaha ya ajabu na kuyasahau magumu ya nyumbani na kumshukuru Mungu.
Mama alinifanya kuona kuwa kanisani na kumwomba Mungu kipindi hicho ndio ilikuwa faraja yetu kubwa na alinisisitiza kuwa nitafanikiwa na kuwa mtu mkubwa katika maisha haya na kunifundisha kusamehe.
Somo la kusamehe lilinikaa sawa sawa na kumsamehe baba yangu kwa kila alichomfanyia mama na kusababisha maisha yetu kuwa magumu hasa baada ya kumpa mama ujauzito uliomfanya aishie kidato cha tatu na kusitisha masomo ili anikuze mimi huku familia yake ikimtenga na kuanza maisha yake.
Nilimsamehe na miezi michache baadae alifariki baada ya kupata tatizo la mapafu yaliyoharibiwa na uvutaji wa sigara na kufa kwa kukosa fedha za kumfanya atibiwe katika hospitali kubwa pamoja na jitihada za kuuza ardhi yetu na baadae maisha yetu yakazidi kuwa magumu.
Nakumbuka kila siku asubuhi nikiwa naenda shuleni jinsi mama alivyonipa nguvu na maneno ya ujasiri yenye uthubutu kuwa nitakuja kufanikiwa na kuitunza familia yetu na pia nakumbuka jirani yetu mama fred ambavyo yeye naye aliwahi kunipa zawadi ya viatu pamoja na ufukara wake ambao ulilingana na ule wetu na kuniambia kila nivaapo vinifanye niamini nitafanikiwa kuyakanyaga maumivu yote na kusonga mbele kufuata sauti ya ushindi na kuja kuwa mtu mwenye mafanikio.
Kila nilipovivaa viatu vile nilihisi kuwa yale maumivu ya mama na maumivu ya ufukara wetu wa kutisha pale kijijini kuna siku ningekuja kuyakanyanga na kumvalisha mama viatu vya furaha na kuja kumfanya maisha yake yote yawe ya furaha na tabasamu kama awapo kwenye kwaya yake siku za jumapili, kwa kweli nilikuwa nikisikia sauti za mafanikio zikiniambia nijitume..
Siku moja tukiwa shule ya sekondari tumekaa kando ya barabara tunacheza na kufurahi mbele yetu alikuja baba mmoja akiwa kashika begi mkononi na mkono mwingine kashika fimbo na miwani jambo lilinifanya nihisi kuwa mzee yule alikuwa ni kipofu.
Akaomba kwa sauti "wanangu naomba mnisaidie kuvuka barabara!"
Hakuna aliyemsikiliza zaidi ya watu kumcheka pale na kuendelea kucheza, mimi nikaamua kusimama na kwenda kumsaidia na nilipofika pale nikamwambia
"naweza kukusaidia?"
Akajibu "ndio"
Nikamwambia naomba nishike bega langu la kulia na nikamvusha na kumbe alikuwa anakuja pale shuleni kwetu na baada ya kuniuliza ni sehemu ipi anaweza kukaa na kumwonesha basi akalifungua lile begi lake na kutoa pipi na biskuti na kuzitandaza juu ya kitambaa chake na kuanza kuziuza na mimi akiniambia,
"mwanangu Mungu atakubariki sana na nitatamani siku nifungue macho yangu kuona mafanikio yako kwani sauti yako tu inanionyesha una hekima na huruma"
Nilimwangalia kwa dakika kadhaa nikiwa pembeni huku akiuza pipi, chocolate na biskuti zake kisha machozi yakanitoka na kushindwa kuyahimili na kuondoka zangu kurejea kwa wenzangu.
Tuliendelea kuwa marafiki na kila siku muda kama ule nilimsaidia kumvusha pale baada ya kuniulizia dan niko wapi, kusikia sauti yangu na mara nyingine alinikuta namsubiri nimvushe pale.
Kuna siku nilifika pale kituoni na kugundua hajafika nikakaa pale kwa dakika kadhaa nikiwa nimejificha sehemu na alipofika nikaaendelea kukaa pale na hakumwita mtu mpaka watu wakaondoka nami nikamsogelea na kukaaa kimya kwa dakika bila kuongea kitu na baada ya watu wachache kupita akaniita "DAN"
Nikaitika nakusema "NAAM", umejuaje kuwa nitakuja na kwanini hujamwomba mtu yoyote akusaidie kuvuka?
Akaniambia " Niliamini kuwa utakuja kwa kuwa wewe ni rafiki na kuna sauti iliniambia lazima utakuja nami nikakusubiri"
Nilishangaa wala sikuongea kitu chochote na kumsaidia kuvuka kisha tukaenda na nikamwacha akiuza nami nikaingia darasani.
Alikuwa rafiki kwani kuna nyakati nilimsaidia hasa pale wanafunzi walipokuwa wakimlipa shilingi mia tano badala ya alfu moja wanunuapo vitu na kunifanya mimi kuwa na maadui wengi pale shuleni zaidi ya marafiki na ikafika kipindi nahitimu pale aliniita na kunipa yeye aliyoiita zawadi ya kuwa
"mwanangu utafanikiwa kama nawe utaisikia sauti ya mafanikio kama mimi nilivyokuwa na imani kuwa kila mara ungenisaidia na ukawa hivyo"
Nilimjibu amen na kuondoka ingawa nilihisi nampoteza rafiki ambaye alinijenga sana.
Miaka miachache baadae kwa jitihada za mama yangu nilifanikiwa kuhitimu chuo kikuu na kupata kazi katika kampuni moja ya kutengeneza vitabu na kipata mwanya wa ufadhili na nikaandika historia ya maisha yangu niliyoiita "Maisha ya Salome na Mwanae Dan" kitabu ambacho kikauzika sana na kunifanya mimi kuweza kumtunza mama.
Nilirudi mpaka ile shule na kumulizia rafiki yangu yule ambaye alikuwa kipofu na kwa bahati mbaya niliambiwa alifariki kwa ajali ya gari baada ya kujitahidi kuvuka barabra kwa kukosa msaada na kugongwa na gari. Nililia sana na kuishia kubaki na yale aliyoniambia na mpaka sasa mimi na mama tuna shirika la kusaidia wajane na walemavu wa macho liitwale "fuata sauti yako foundaton"
Kwa nini nimetaka kuandika kisa hiki cha kufikirika?
Kila mtu ana historia ya mapito magumu katika maisha yake na pengine hata sasa una wakati mgumu sana na hujui nini cha kufanya.
Hebu fikiri wakati mama yangu ananyanyasika na kufanya kazi kwa taabu ili kunipa maisha mimi aligundua kuwa ana tone la furaha na kulitumia ipasavyo hasa zile nyakati za kwenda kanisani na kuimba na wenzake na kusahau maumivu ya muda na kujipanga kuona atayakabili vipi.
Mama Fred yeye hakuwa na fedha sana na alikuwa ni maskini kama sisi lakini vile viatu ambavyo alinunua na kunipa pamoja na yale maneno mazuri vilinihamasisha kufanya vizuri. Je wewe umekuwa msaada kwa wenzako hata kama na wewe unaona huna kitu? Umewapa maneno ya faraja au umekuwa ukifurahia magumu yao?
Yule kipofu aliomba msaada na wengi wakawa wakimwangalia na kumcheka je ni mara ngapi na wewe umeomba msaada na watu na kuchukulia ni utani na kuja kujutia baada ya kugundua kuna mtu ulishindwa kumsaidia katika nyakati aliyohitaji msada wako?
Ni mara ngapi umewasamehe wale waliokufanyia mabaya na hata kuwafanyia mabaya wale uwapendao mbele yako kama nilivyomshuhudia baba akimnyanyasa mama na mwisho wa siku nikamsamehe ingawa alifariki baadae hata kabla ya kuja kula mafaniko ya mwanae?
Ni mara ngapi umesaidiwa na kuwa na shukrani hata ya maneno mazuri kama vile yule kipofu alivyomfanyia dan na hata kujenga imani ya kuwa huyo mtu aliyekusaidia unahitaji kumwamini na kuuthamini mchango wake?
Ni mara ngapi umerudi kuwashukuru wale waliokusaidia nyakati za shida au ulivyowahitaji wakusaidia na wakakusaidia?
Katika kufanikiwa kwako au katika jitihada za mafanikio yako umefuata sauti liyomo ndani yako kuwa utafanikiwa na ukaishi kwa ndoto zako huku ukijituma na kujikabidhi kwa mungu ?
Baada ya kila dhoruba kali nuru huonekana ....... nakutakia wiki hii kuwa ya mafanikio kwako......AMEN-------------> share ------------>

You Might Also Like

0 comments: