NATAMANI NINGESIKILIZA MANENO YA MAMA YANGU

05:22:00 Unknown 0 Comments

Ilikuwa mara ya kwanza kwa mimi kupigiwa simu na Jane mchana kama kama ule huku akionyesha kufurahi kuliko kawaida yake.

Baada ya kuniambia aliko nikaenda haraka na nilipofika pale nikaonana naye akiwa na rafiki yake ambaye alinitambulisha kuwa ni nesi wa hospitali moja binafsi.

Wakati nikijiandaa kukaa akanirushia mkononi kikaratasi chenye majibu ya daktari na kuonyesha ana mimba ya wiki sita.

Kwa furaha nilimrukia na kumbusu na kisha kuomba mhudumu aniletee whisky niweze meza fundo kadhaa kwa kuashiria kufurahia habari zile.

Ni kweli mimi na jane tulioana miaka minne iliyopita pamoja na baadhi ya ndugu zangu kunikanya niachane nae ila mimi nikabaki na msimamo na kukaa naye.

Na kwa miaka miwili nilikuwa sina mahusiano mazuri na dada zangu, mama yangu na baadhi ya ndugu wakidai kuwa nitaendeleaje kuishi na mtu asiyezaa.

Tuachane na hayo ila kwa habari niliyoipokea siku hiyo nikaona kuna kila dalili za furaha hasa ukivuta picha ya kuanza kuitwa baba......we acha tu.

Nilifurahia sana nyakati zile pamoja na kuanza kuexperience mambo mapya kama vile jane kuanza  kudeka, kuchagua vyakula,  mara kila wakati niwepo jirani naye na wivu kuzidi mpaka nikakoma ila kwangu ikikuwa burudani.

Baada ya miezi mitatu akaomba aende kwa rafiki yake yule nesi kwa kuwa alihamishiwa kijijini ili akajingojelee.

Nilikataa kabisa ila wakasisitiza kwa pamoja yeye  na rafiki yake wakidai kwa kuwa ni mimba ya kwanza hivyo aende akapate msaada wa karibu kwa kuwa huyo ni nesi mtaalamu wa masuala wanawake wajawazito.

Sio mimi tu niliyeugomea uamuzi wa jane kwenda kijijini kule bali hata wazazi wangu na wake walikuwa wakigomea uamuzi huo ila yeye akasimamia uamuzi wake jambo lililotufanya tuafikiane nae ingawa kwa shingo upande.

Akaenda na kuanza kukaa huko nami nikawa kila mwisho wa wiki nikienda na kushuhudia tumbo likianza kuwa kubwa jambo lililonipa faraja na kujiona mbarikiwa.

Jambo la ajabu ni kwamba sikupewa nafasi ya kulala na mke wangu akidai ni ushauri wa nesi kitu kilicho nishangaza ingawa ikanibidi nivumilie.

Lakini siku zilivyozidi kwenda kila nikijitahidi kuvumilia nikashindwa kwani nami nilitamani kushika tumbo na kuona mapigo ya mwanangu wa pekee na hata kuongea nae kwa hisia kama kina baba wengine hasa ndugu zangu na marafiki pindi wake zao walipokuwa wajawazito jinsi walivyofurahia.

Nikaamua kumshirikisha rafiki yangu suala hili nae akadai labda kuna jambo nichunguze vyema... Hivyo nimchukue jane na kumpeleka kwa daktari mwingine ili nijue kuna nini?

Jane alikataa katakata akidai au simwamini na kama simpendi nimwambie maana naanza kufanya mambo ya ajabu na ya kumdhalilisha.

Hali ile ikanitia hofu zaidi na kuamua kwenda kwa dada yangu wa tumbo moja tuliyependana sana na kuaminiana kwa kila jambo.

Baada ya kumshirikisha akaniambia hapo kuna jambo basi akaniomba jumamosi yake nimsindikize mpaka kule aliko jane ili nae amwone.

Dada alifika pale na jane akaonyesha hali ya hofu na dada akamwambia wewe usinidanganye kwa utu uzima wangu huu wewe huna mimba....

Nikawa najaribu kumkataza dada asiongee maneno hayo kwani kwa mama mjamzito ni mabaya yanaweza kumfanya awe na mawazo au hasira na kuhatarisha afya na mtoto aliye tumboni.

Dada akanyanyuka na kwenda kumshika tumbo wakati huo yule rafiki wa jane akawa anatetemeka na kuonyesha hana amani jambo lililonipa nguvu ya kusimama na kwenda kumchunguza jane kwa makini.

Amini usiamini kumbe muda wote huo jane kafunga vitambaa tumboni ili tujue ana mimba kumbe sio.

Nikamchukua na kumpeleka kwa daktari na kufika pale kwa bahati nzuri ni daktari ninayemfahamu nilipomwomba atupime kama tuna uwezo wa kuzaa akanivuta na kusema mbona last time shem jane amekuja nilimpima na kusema kwa sasa hawezi kupata mtoto? Kwani hakukuambia?

Kumbe jane alishatoa sana mimba enzi za ujana wake na kuharibu kizazi.

Nikajiuliza sasa jane mwisho wa maigizo yale angeniletea mtoto toka wapi??????

Tumeachana nae ila nashindwa hata kuwa na nguvu ya kumwamini mwanamke yoyote tena hapa duniani.

NATAMANI NINGESIKILIZA MANENO YA MAMA YANGU

Weka tabgazo la bure kwenye blog hii

Wasiliana Whatsapp 0713317171

You Might Also Like

0 comments: